Saturday, 24 January 2015

NITAENDELEZA NDOTO ZA KANUMBA......................

Dar es Salaam. Mama wa aliyekuwa nyota wa filamu nchini, marehemu Steven Kanumba, Flora Mtegoa amesema kuwa kupitia Kampuni ya Kanumba The Great Film inakamilisha uanzishaji wa taasisi itakayoitwa, Kanumba Foundation.
Pia, alikanusha uvumi kuwa kampuni ya Kanumba imekufa, akifafanua jambo hilo alisema kampuni hiyo inaendelea na shughuli zake. Alisema kutakuwapo Kanumba Foundation ili kusaidia jamii wakiwamo wasanii katika masuala mbalimbali.
Akizungumza na gazeti hili, Flora alisema uamuzi wa kuanzisha taasisi hiyo ni kuendeleza na kutimiza ndoto alizokuwanazo mtoto wake, marehemu Steven Kanumba enzi za uhai wake.
"Tunaanzisha Kanumba Foundation. Awali haikuwapo, tulivyojaribu kulikuwa na mlolongo mrefu, marehemu Kanumba alikuwa na mipango mingi, huo ukiwemo. Kanumba alisema akisharejea safari yake ya Marekani kuna vitu atafanya, lakini Mungu akampenda zaidi," alisema Flora na kuongeza:
"Mipango yake ilikuwa ni kuanzisha chuo kikubwa cha kufundisha sanaa ya uigizaji kwa kuwachukua waigizaji chipukizi na kuwafunza ili wawe bora." Kuhusu Kampuni ya Kanumba The Great, Mtegoa ambaye pia ni msanii alisema licha ya kusema kuwa kampuni hiyo imekufa, lakini mpaka sasa imeweza kutengeneza filamu kadhaa.
"Kampuni ipo na bado naendelea kuisimamia. Kwa kipindi chote imetengeneza filamu mbili ambazo zilishapelekwa sokoni tangu mwaka jana. Watu wengi wanaamini kwamba ilifungwa, ila ipo na ina watu kama kawaida, japokuwa ukipita nje unaona kama imefungwa," alisema. Flora maarufu kwa jina la Mama Kanumba, alifafanua kwamba kampuni hiyo imekuwa ikifanya kazi za watu wengine, pia inatengeneza filamu zake yenyewe. Alisema kutokana na uwepo wa kampuni hiyo wameweza kufanya mambo mengi, ikiwamo kutimiza ndoto za marehemu Kanumba za kuwa na mfuko wa jamii.
Akizungumzia kipaji chake cha uigizaji, Mama Kanumba alisema hakufanya hivyo baada ya mwanaye kufariki, bali alikuwa akiigiza wakati alipokuwa kigori, hivyo ameamua kuendeleza kipaji chake.
"Nikiwa sekondari niliigiza, wakati huo mtoto wa kike kupelekwa shule mpaka vikao, zamani binti hakuruhusiwa kusoma, ilikuwa ngumu, kwa hiyo unacheza huku ukifikiria kwamba nyumbani wakijua nimeingia huku itakuwa tatizo, baadaye nikaacha," alisema.
Alisema baada ya Kanumba kufariki, aliamua kuendeleza kipaji chake kwa kutumia rasilimali alizoachiwa na mtoto wake.CHANZO:MWANANCHI

No comments:

Post a Comment