Ndugu zangu,
Leo ni
Siku ya Mashujaa. Nimeangalia TBC1 leo wakionyesha tukio lile la
kihistoria pale nchi yetu ilipowapokea rasmi mashujaa wetu wa Vita Vya
Kagera. Nilikuwa miongoni mwa watoto wale pale National Stadium.
Nilikuwa na miaka 13 tu.
Ilikuwa
ni siku ya ajabu, maana, shughuli nzima iliingia doa pale kwa macho yetu
tuliposhuhudia ndege yetu ya kijeshi ikianguka na kuwaka moto. Hakika,
rubani yule alifanya kazi ya kijasiri na kizalendo sana, maana,
ingewezekana kabisa ndege ile kuangukia uwanjani na kusababisha madhara
makubwa.
Nakumbuka
kuiona ndege ile ikishuka huku ikitoa moshi, haikuwa jambo la kawaida.
Hata katika umri wangu ule mdogo, nikahisi kuna kitu hakijaenda sawa.
Mara tukaona ikikwepa kuangukia uwanjani na kuanguka nje ya uwanja.(P.T)
Nakumbubuka
kushuhudia uwanja ukikumbwa na butwaa, mara zikasikika sauti za watu
wakipiga kelele, kuna tulioanza kukimbilia eneo la tukio, kwa shauku ya
kujua nini kimetokea, nami nilikuwa mmoja wao. Lakini sikufika mbali,
nikarudi nilikosimama, chini na jirani na jukwaa kubwa.
Na hata
aliyekuwa Waziri wa Ulinzi, Rashid Kawawa, alikuwa ni mmoja wa viongozi
walioshuka jukwaani akikimbia, naye alionekana aliyeshtushwa, na pengine
alilazimika kushuka jukwaani kwa vile alikuwa ni waziri mwenye dhamana
ya Ulinzi. Rashid Kawawa alikuwa akiwajibika kwenye kazi yake.
Sura ya
Rais, Julius Nyererere ilikuwa imevaa huzuni kubwa. Na aliposimama
kuzungumza, napo ilikuwa ajabu kwangu katika umri ule, kuwa Julius
Nyerere hakusema lolote juu ya tukio lile.
Lakini
hii leo, nilipokuwa nikiangalia tukio la siku ile kupitia TBC1, nimekuwa
mwelewa zaidi, kuwa Julius Nyerere alisiama kama Mkuu wa Nchi,
alilijumuisha tukio lile na mashujaa wengine waliojitoa muhanga kwa
ajili ya nchi yetu. Julius Nyerere hakushuka chini na kuzungumzia tukio
la kuanguka kwa ndege ile. Badala yake,alitoa hotuba muhimu kwa taifa
baada ya vita. Na ni katika siku ile Julius Nyerere alitangaza miezi
kumi na nane ya kufunga mkanda.
Na hakika, makovu ya kiuchumi ya Vita Vya Kagera yangalipo mpaka hii leo. Naam, Vita Si Lelemama.
Maggid Mjengwa,
Dar es Salaam.
Dar es Salaam.
No comments:
Post a Comment